Jinsi Urusi inavyofanya kampeni katika maeneo yaliyovamiwa ili kuhamasisha watu kujiunga na jeshi lake
Juhudi hizi zinalenga kuongeza idadi ya wanajeshi katika jeshi la Urusi kwa ajili ya vita dhidi ya Ukraine. Ili kufanikisha hilo, mamlaka bandia hutumia mbinu mbalimbali za ushawishi na njia tofauti za mawasiliano.
Endelea kusoma ili kupata muhtasari wa jinsi wakazi wanavyohimizwa kujiunga na jeshi, pamoja na mbinu za uajiri na zana za propaganda zinazotumika kwa sasa.
Uhamasishaji wa kulazimishwa
Baada ya kutekwa kwa Mikoa ya Luhansk na Donetsk, hatua ya awali ya Urusi ilikuwa kuwaweka wakazi wa eneo hilo katika sajili za kijeshi, kabla ya kuwalazimisha kujiunga na Vikosi vya Wanajeshi wa Shirikisho la Urusi ili kupigana dhidi ya Ukraine.
Hata kabla ya uvamizi kamili, tarehe 19 Februari 2022, mamlaka za uvamizi zilitoa amri iliyoitwa “Kuhusu Uhamasishaji wa Jumla.” Amri hiyo inawahusu wanaume wote walio katika umri wa kusajiliwa jeshini, pamoja na wanawake katika taaluma fulani.
Kulingana na wakazi, watu waliovalia sare huwapatia watu hati za wito wa kujiunga na jeshi mitaani na katika maeneo ya kazi, huku pia wakiwatembelea majumbani.
Zaidi ya hayo, vikosi vya uvamizi huendesha misako katika maeneo ya umma yenye mikusanyiko ya watu ili kuwakamata wanaume na kuwapeleka katika vituo vya ‘mafunzo’ ya kijeshi.
Mkazi mmoja wa Rubizhne aliyefanikiwa kutoroka kutoka eneo lililovamiwa alielezea hali ya watu waliohamasishwa katika Mkoa wa Luhansk:
‘Miongoni mwao kuna wavulana wengi wenye umri wa miaka 17 na 18 na wafanyakazi wa kawaida wa viwandani ambao hawakuwa wamewahi kushika bunduki hapo awali. Wote wangependa kurudi nyumbani na hawataki kupigana. Wengi walipelekwakatika mstari wa mbele, na nina shaka kama wengi wao bado wako hai.’
Katika kituo cha ukaguzi cha Uspenka, kilichoko katika Mkoa wa Donetsk uliovamiwa na Urusi kwenye mpaka na Urusi, wanaume ambao pasipoti zao hazina muhuri wa usajili wa kijeshi hupewa hati za wito wa kujiunga na jeshi mara kwa mara wanapovuka mpaka. Kwa sababu hiyo, wakazi wengi wa eneo hilo huepuka kituo hiki cha ukaguzi.
Kampeni za uajiri miongoni mwa wakazi wa eneo hilo
Pamoja na uhamasishaji wa kulazimishwa, Urusi inaendesha kikamilifu kampeni za kuwahimiza wakazi wa eneo hilo kujiunga na jeshi lake, ikitegemea zana za propaganda na njia za mawasiliano ili kuonyesha taswira nzuri ya huduma ya kijeshi.
Kampeni hizi zinalenga kuathiri mitazamo, kuonyesha huduma ya kijeshi kama fursa ya kutatua matatizo ya kijamii au kifedha, na kuhamasisha watu kujiunga kwa kutumia kaulimbiu za ‘uzalendo’ na ‘kulinda Nchi yao.’
Mabango, matangazo na vipeperushi
Kando ya barabara katika miji na maeneo ya makazi yaliyovamiwa katika Mikoa ya Luhansk na Donetsk, mabango yanawahimiza wakazi kujiunga na huduma ya kijeshi kwa mkataba katika Vikosi vya Wanajeshi vya Urusi. Yanatumia kaulimbiu kama “Chaguo lako” au “Ushindi utakuwa wetu.” Ahadi za malipo ya kifedha hutumiwa kuvutia umakini wa watu.
Aidha, mabango hayo huonyesha maelezo ya mawasiliano ya vituo vya uajiri, yanaeleza mafao yanayodaiwa kupatikana kupitia huduma ya kijeshi kwa mkataba, na yana picha za wanajeshi wa Urusi.
Vipeperushi vya propaganda vyenye kaulimbiu ‘Tuhudumu pamoja’ huwekwa katika maeneo mbalimbali ya miji, vikieleza kwamba ofa hiyo inahusu huduma ya kijeshi kwa mkataba na kuorodhesha mafao yanayodaiwa kupatikana.
Vipeperushi vyenye kichwa ‘Hudumu kwa mkataba katika vikosi vya kijeshi’ hutolewa kwa wakazi, vikiwa na maelezo kuhusu sifa zinazohitajika kwa waombaji, malipo ya kifedha, mafao ya kijamii na dhamana zinazotolewa.
Gumzo za ndani za Telegram
Urusi inategemea kwa kiasi kikubwa gumzo za ndani za Telegram katika maeneo yaliyovamiwa ili kusambaza wito wa kujiunga na jeshi. Ujumbe hujitokeza mara kwa mara ukiwahimiza wakazi kujiunga na Vikosi vya Wanajeshi vya Urusi na kushiriki katika mapigano dhidi ya Ukraine.
Tangazo moja linatoa nafasi za kazi katika vikosi vya ulinzi wa anga, likiahidi malipo ya rubles 1,000,000 (EUR 10,700) baada ya kusaini mkataba. Ofa hiyo inalenga wanaume wenye umri wa miaka 18 hadi 45.
Katika machapisho mengine yanayofanana, kaulimbiu za propaganda zina jukumu muhimu: ‘Kuna taaluma kama hii — mtetezi wa Nchi,’ ‘Jiunge na watu wako katika SMO!’ na ‘Hatuwaachi watu wetu.’
Kauli kama hizi hujenga taswira potofu ya ‘umoja’ na kuwa sehemu ya kundi, huku zikichochea hisia ya ‘wajibu wa kiraia’ ili kuwahamasisha watu kujiunga na jeshi.
Video za mitandao ya kijamii
Video ni miongoni mwa zana za kisasa zaidi za propaganda, na hutumiwa kwa ufanisi kuathiri wakazi wa maeneo yaliyovamiwa. Vyanzo vya Urusi haviishii tu kuwahimiza watu kutia sahihi mikataba na vikosi vyao vya kijeshi; pia hutumia mbinu za kuchochea hisia kupitia video za mapigano na simulizi zinazolenga jamii.
Kwa mfano, video moja ya mitandao ya kijamii inaonyesha kikosi cha ‘BARS-LPR’, kikiwahimiza watu kujiunga na jeshi kwa kaulimbiu ‘Kulinda anga za Mkoa wa Luhansk.’ Video hiyo inaonyesha operesheni za kivita pamoja na vipande vya video vinavyodaiwa kuwaonyesha wanajeshi wakiwasaidia wakazi wa eneo hilo.
Video nyingine ya kampeni inahamasisha huduma ya kijeshi kupitia simulizi binafsi za wanaume waliosaini mikataba ‘kwa hiari.’ Inaonyesha picha za mafunzo yao ya kijeshi huku ikisisitiza umuhimu wa kutimiza ‘wajibu’ wa mtu kwa serikali, na kumalizia kwa kaulimbiu: ‘Simameni bega kwa bega na watu wenu katika SMO!’
Taasisi za elimu na ujeshi wa vijana
Katika maeneo yaliyovamiwa ya Mikoa ya Luhansk na Donetsk, Urusi inalenga kikamilifu wanafunzi ili kuwahamasisha kujiunga na jeshi la Urusi, na kuunda mazingira yanayowachochea vijana kujiunga na vikosi vinavyopigana dhidi ya Ukraine.
Katika taasisi za elimu ya juu kote katika Mkoa wa Luhansk uliovamiwa na Urusi, wanafunzi wanaofukuzwa hupewa likizo ya masomo kwa sharti kwamba wasaini mkataba na jeshi la Urusi. Baadhi yao wametishiwa kufukuzwa na baadaye kulazimishwa kujiunga na jeshi isipokuwa wakubali ‘kwa hiari’ kuhudumu.
Aidha, baadhi ya taasisi huendesha kozi za kijeshi kwa vijana na kuandaa mikutano na wanajeshi wa Urusi. Matukio haya yanajenga mtazamo chanya kuhusu huduma ya kijeshi, yanasisitiza ‘uzalendo,’ na kuhamasisha ushiriki katika operesheni za kivita upande wa Urusi.
Kampeni za uajiri pia zinalenga wanafunzi wa shule. Kupitia vipindi vya ushauri kuhusu taaluma, wanafunzi hufundishwa wazo la kujiunga na taasisi za elimu ya kijeshi.
Makosa yanayopelekea kutia sahihi mkataba na jeshi la Urusi
Kwa mujibu wa mtu anayeishi chini ya uvamizi, pamoja na hatua hizi, kuna mpango wa kuwalazimisha wahalifu kujiunga na jeshi la Urusi:
‘Wale ambao “vyombo vya sheria” haviwezi kufikia makubaliano nao, au wale wanaotaka kujinufaisha kutokana nao, wanalazimishwa kusaini mkataba.’ Baada ya hapo, wanapelekwa katika vitengo vya kijeshi, ambako wengi wao hufa haraka.’
Urusi inatafuta kuajiri watu wengi iwezekanavyo katika jeshi lake — wakiwemo raia wa kigeni kutoka nchi kama Kenya — ili kupigana dhidi ya Ukraine. Wakati huohuo, operesheni zake za propaganda katika Mikoa ya Luhansk na Donetsk iliyovamiwa zinaonyesha mkusanyiko mpana wa zana na njia za mawasiliano.
Mabango, vipeperushi, machapisho kwenye mitandao ya kijamii na gumzo za Telegram, video fupi, pamoja na matumizi ya taasisi za elimu, yote ni sehemu za mfumo mmoja wa kuwaajiri watu katika jeshi la Urusi. Kuchanganua mbinu hizi kunatoa mwanga kuhusu mifumo mahususi ya propaganda ambayo Urusi hutumia kuwashawishi watu kujiunga na vita, na kunasaidia kubuni hatua za kukabiliana na kampeni kama hizo.