Chakula Chini ya Udhibiti

Jinsi utekwaji wa Mariupol ulivyofanya eneo la kusini mwa Donetsk kutegemea Urusi

Baada ya kutekwa kwa Mariupol, Urusi haikubadili tu mamlaka, hati na bendera za jiji hilo. Ilivunja pia mojawapo ya mifumo ya msingi ambayo maisha ya kila siku ya watu hutegemea: upatikanaji wa chakula.

Minyororo ya usambazaji wa chakula ya Ukraine ilikatizwa. Mitandao ya rejareja iliyokuwapo kabla ya vita ilitoweka au ilianza tena kufanya kazi kwa majina tofauti. Rafu za maduka zilijazwa bidhaa kutoka Urusi na Belarus. Bei, usafirishaji wa bidhaa na hata uwezo wa kufikisha chakula katika makazi yanayozunguka jiji hilo ulizidi kutegemea mifumo ya usafirishaji, mafuta na maamuzi ya utawala wa uvamizi wa Urusi.

Kwa mtazamaji wa nje, Mariupol ya leo inaweza kuonekana kama jiji ambalo maduka yanafanya kazi na chakula kinapatikana kwenye rafu. Hivyo ndivyo mamlaka za uvamizi zinavyojaribu kuwasilisha taswira ya kile wanachokiita "urejeshaji wa hali ya kawaida." Lakini usalama wa chakula haupimwi kwa kuangalia picha ya rafu za duka kubwa. Unahusu nani anayesimamia barabara, maghala, wasambazaji, mafuta, maeneo ya biashara za rejareja, bei za bidhaa na uwezo wa watu kununua kikapu cha kawaida cha mahitaji ya chakula.

Dhamana za Kisheria za Usalama wa Chakula

Kwa mujibu wa Benki ya Dunia, usalama wa chakula ni hali ambayo watu wanaweza kupata chakula cha kutosha, salama na chenye lishe bora, kwa urahisi wa kimwili na uwezo wa kiuchumi. Katika Mariupol iliyotekwa, upatikanaji huo umekuwa katika hatari tangu mwaka wa 2022.

Urusi ilibadilisha mfumo wa usambazaji wa chakula wa Ukraine na kuweka mfumo uliofungwa unaotegemea wasambazaji, njia za usafirishaji, mafuta na mifumo ya usafirishaji ya Urusi.

Minyororo ya Usambazaji ya Ukraine Ilibadilishwa na ya Urusi

Kabla ya vita kamili kuanza, Mariupol ilikuwa sehemu ya mfumo wa uchumi wa Ukraine. Chakula kilisafirishwa kutoka maeneo mbalimbali ya nchi, huku mitandao ya biashara za rejareja, masoko, maghala ya usambazaji na wakulima wa maeneo ya jirani wakihudumia jiji hilo. Baada ya uvamizi na kutekwa kwa jiji hilo katika majira ya kuchipua ya mwaka wa 2022, mfumo huo ulisambaratika. Maduka na maghala yaliharibiwa, wafanyabiashara waliondoka, mali zilichukuliwa na kuendeshwa na waendeshaji wapya, huku bidhaa za Urusi zikianza kutawala soko.

0629.Com.ua iliripoti kuwa usambazaji wa chakula na bidhaa za usafi uliwekwa chini ya udhibiti wa kampuni za Urusi na husafirishwa kupitia mkoa wa Rostov na eneo la Krasnodar nchini Urusi. Minyororo ya usambazaji ya Ukraine, maghala na njia za usafirishaji zilipobadilishwa na zile za Urusi, wananchi walipoteza njia mbadala na kulazimika kutegemea mfumo uliofungwa wa utawala.

Utafiti wa “Looting Mariupol” wa SOC ACE / RUSI unaeleza kuwa uwekezaji wa Urusi umeambatana na unyakuzi usio halali wa maelfu ya nyumba, biashara na mali za Waukraine. Usalama wa chakula pia unategemea umiliki wa mali, maghala, njia za usafirishaji, upatikanaji wa mafuta na vibali vya kufanya biashara.

Image
Not yours, that's why you are seething

Chakula kinapatikana, lakini upatikanaji wake unazidi kuwa mgumu

Kulingana na Novyny Donbasu, RIA Pivden and 0629.com.ua, katika mwaka wa 2025, lita moja ya maziwa ya kienyeji huko Mariupol iliuzwa kwa takriban ruble 100 za Urusi, mayai yalikuwa ruble 150 kwa dazeni, jibini kati ya ruble 250 na 300, na krimu nzito ruble 350. Wakazi wanasema kuwa katika mwaka wa 2026, bei za bidhaa za msingi ziliongezeka kwa angalau robo moja, jambo lililofanya iwe vigumu zaidi kwa wastaafu na familia zenye watoto kumudu lishe ya kawaida.

Viktoria Sh., mwenye umri wa miaka 58, ameishi Mariupol tangu kuzaliwa. Kabla ya mwaka wa 2022, alinunua chakula katika soko la karibu: maziwa ya vijijini, mayai kutoka kwa wakulima na nyama mara moja au mbili kwa wiki. "Siwezi kusema kwamba tulikuwa matajiri, lakini tuliweza kujitosheleza. Ningeweza kununua jibini, kuku, mboga na bado kubaki na pesa kidogo," anakumbuka.

Baada ya utekwaji, sehemu ya soko ilisitisha shughuli zake, wafanyabiashara wengi waliondoka, na maduka yaliyouza bidhaa za Urusi yakaanza kuibuka. "Maziwa yakawa ghali zaidi na si yale tuliyozoea. Mayai vilevile. Zamani nilikuwa nanunua dazeni mbili au tatu bila kufikiria, lakini sasa lazima nihesabu kama yatatosha kwa wiki nzima," anasema Viktoria.

Sasa hununua nyama, mboga na matunda mara chache zaidi kuliko hapo awali. "Zamani nilijua kwamba ningeweza kununua kile nilichohitaji. Sasa sijui kitakachotokea kesho. Hicho ndicho kinachonisumbua zaidi," anasema.

Mafuta, barabara na bandari: Mifumo ya usafirishaji chini ya uvamizi

Katika Mariupol, upatikanaji wa chakula unahusiana moja kwa moja na mifumo ya usafirishaji na upatikanaji wa mafuta. Jiji hilo linategemea njia za usafirishaji zinazopitia Urusi na maeneo ya kusini mwa Ukraine yaliyotekwa. Mnamo Juni, 0629 reported iliripoti kuwa huduma moja ya usafirishaji wa bidhaa iliwapa wateja fursa ya kumlipa mtoa huduma za usafirishaji lita moja ya petroli badala ya ada ya usafirishaji. Mwanzoni mwa Julai, bei ya petroli aina ya A-92 na A-95 ilipanda hadi kati ya ruble 150 na 170 kwa lita.

Vyanzo katika mkoa wa Donetsk uliotekwa vinasema kuwa barabara ndizo eneo kuu ambalo Urusi imewekeza kwa ajili ya mifumo ya usafirishaji wa kijeshi katika mstari wa mbele wa mapigano. Utafiti wa SOC ACE / RUSI pia unaeleza Mariupol kama kituo kikuu cha usafirishaji kwa jeshi la Urusi na kwa usafirishaji haramu wa bidhaa nje ya eneo hilo. "Lo, Warusi wanajenga barabara vizuri sana," wakazi husema. Hata hivyo, barabara hizo ni sehemu ya miundombinu ya usafirishaji wa kijeshi, jambo linalowafanya raia kutegemea mfumo unaohusishwa na shughuli za vita katika mstari wa mbele.

"Warusi hawajaweza kuanzisha matumizi ya takriban asilimia 60 ya vifaa vya bandari. Hakuna umeme wa kutosha kuendesha kreni," anasema Mykola D., ambaye bado anaishi katika eneo lililotekwa na alikuwa akifanya kazi bandarini kama mpakiaji wa mizigo kabla ya uvamizi.

Katika mwaka wa 2026, Rosselkhoznadzor ya Urusi iliripoti kuwa kati ya Januari na tarehe 8 Juni, meli 12 zilizobeba karibu tani 90,000 za ngano ziliondoka katika Bandari ya Mariupol kuelekea nchi mbalimbali, zikiwemo baadhi ya mataifa ya Afrika na Asia. Takwimu hizi zinaonyesha hali kinzani: wakati nafaka kutoka maeneo ya Ukraine yaliyotekwa zinaendelea kusafirishwa nje kupitia Bandari ya Mariupol, usambazaji wa chakula kwa wakazi wa jiji hilo unazidi kutegemea bidhaa zinazoagizwa kutoka Urusi. Hali hii inaonyesha jinsi utekwaji ulivyobadilisha biashara za ndani na mfumo wa biashara wa eneo nzima. 

Utegemezi huu ni mkubwa zaidi katika maeneo ya Manhush, Nikolske, Urzuf, Yalta, Yuriivka na Staryi Krym, ambako kuna maduka machache, ushindani mdogo wa kibiashara na utegemezi mkubwa wa barabara na upatikanaji wa mafuta.

Kabla ya vita, Leonid na Nadiia kutoka Nikolske walikuwa na shamba ndogo na kila mwishoni mwa wiki walikuwa wakipeleka maziwa, jibini, mayai, nyama na mboga mjini Mariupol kwa ajili ya kuuza. "Hapo ndipo tulipokuwa tukipata riziki yetu," anasema Leonid. "Watu walitufahamu na walikuwa wananunua bidhaa zetu mara kwa mara."

Baada ya mwaka wa 2022, shamba lao liliendelea kuwepo, lakini mfumo wao wa maisha ulitoweka. "Hatuendi tena Mariupol," anasema Nadiia. "Kuna vizuizi vya ukaguzi na masharti ya hati. Watu pia wana pesa chache sasa, hivyo wanaulizia bidhaa za bei za chini pekee."

"Tunatumia pesa kununua petroli, tunakaa huko kwa nusu siku, halafu tunarudi na karibu bidhaa zilezile tulizoenda nazo. Zamani ilikuwa biashara yenye faida; sasa ni hatari," anasema Leonid. Kwa sasa, huuza bidhaa zao sanasana katika Nikolske na katika vijiji vya jirani.

Utegemezi badala ya uthabiti

Mfano wa Mariupol unaonyesha jinsi utekwaji unavyobadilisha maisha ya kila siku. Maduka yanaendelea kufunguliwa, lakini yako chini ya umiliki mpya, yanatumia majina tofauti, na rafu zake zinazidi kujazwa bidhaa kutoka Urusi. Gharama za usafirishaji zimeongezeka, huku uvamizi wa Urusi katika bandari, ambayo hapo awali ilikuwa lango muhimu la usafirishaji wa nafaka kutoka maeneo ya Ukraine kwenda nje ya nchi, ukiinyang'anya Ukraine udhibiti wa sehemu muhimu ya miundombinu yake ya mauzo ya nje. Hali hiyo imepunguza mapato yatokanayo na mauzo ya nje na kuendelea kudhoofisha uchumi wa nchi. Mamlaka za utekwaji za Urusi huwasilisha hali hii kama "kurejesha hali ya kawaida." Lakini kwa mtazamo wa usalama wa chakula, kinachojengwa ni mfumo wa utegemezi, ambapo upatikanaji wa chakula unadhibitiwa na mamlaka za nje. Kimsingi, maduka na bidhaa bado zipo katika jiji. Lakini upatikanaji wa chakula ulio thabiti na wa uhakika umepotea.