Vita na Biashara: Jinsi Uvamizi wa Donbas Ulivyoathiri Uhusiano wa Kiuchumi wa Ukraine na Kenya na Malaysia

Kwa zaidi ya miaka 30, Ukraine imekuwa ikiendeleza uhusiano wa kibiashara na kiuchumi na Jamhuri ya Kenya na Malaysia. Bidhaa za kilimo na metallojia zilikuwa na nafasi muhimu katika mauzo ya nje ya Ukraine kwenda katika nchi hizi. 

Biashara na sekta ya kilimo katika mikoa ya Donetsk na Luhansk zilitoa mchango mkubwa katika kujenga uwezo huu wa kuuza bidhaa nje ya nchi. Hata hivyo, vita vilivyoanzishwa na Urusi katika mwaka wa 2014, vikifuatiwa na uvamizi kamili, vilisababisha kupotea kwa uwezo wa uzalishaji, kuharibiwa kwa minyororo ya ugavi, na mabadiliko katika muundo wa biashara ya nje ya Ukraine.

Makala hii inachunguza jukumu ambalo mikoa ya Luhansk na Donetsk ilichukua katika ushirikiano wa kiuchumi wa Ukraine na Kenya na Malaysia, jinsi vita hivyo vilivyoathiri uwezo wa kuuza nje wa eneo hilo, na athari zake kwenye uhusiano wa kibiashara wa Ukraine na nchi hizi.

Biashara na ushirikiano wa kiuchumi kati ya Ukraine, Kenya na Malaysia

Kwa miaka mingi ya ushirikiano wa kiuchumi, Ukraine iliuza sanasana bidhaa za kilimo na metallojia kwenda Kenya na Malaysia. Bidhaa kuu zilizokuwa zikiuzwa nje zilijumuisha metali za feri, mazao ya nafaka, mafuta ya mimea, pamoja na mboga. Wakati huo huo, Ukraine iliagiza kahawa, chai, matunda, tumbaku, kakao na bidhaa za kakao, mashine za umeme na bidhaa nyingine. Muundo na kiwango cha biashara kati ya nchi hizo mbili kilibadilika kulingana na maendeleo ya sekta mbalimbali na mahitaji katika masoko ya nje.

Biashara na sekta ya kilimo katika mikoa ya Donetsk na Luhansk zilikuwa na nafasi kubwa katika kujenga uwezo wa Ukraine wa kuuza bidhaa nje. Hasa, viwanda vya chuma vya Azovstal, Illich na Alchevsk vilizalisha bidhaa za metallojia ambazo zilikuwa sehemu muhimu ya mauzo ya nje ya Ukraine, ikiwemo kwenda Asia na Afrika — haswa Kenya na Malaysia.

Mikoa ya Donetsk na Luhansk pia ilikuwa miongoni mwa wazalishaji wakuu wa ngano, mahindi, mbegu za alizeti na mafuta ya alizeti. Uzalishaji huo uliwakilisha sehemu kubwa ya jumla ya uzalishaji wa Ukraine na ulitumika kusafirisha bidhaa kwenda katika nchi hizi.

Hata hivyo, uvamizi wa kijeshi wa Urusi ulioanza katika mwaka wa 2014 na uvamizi kamili wa mwaka wa 2022 ulisababisha pigo kubwa kwa uwezo wa Ukraine wa uzalishaji wa viwandani na kilimo, hasa katika mikoa ya Luhansk na Donetsk. Kutokana na vita, viwanda viliharibiwa au kuathiriwa, maeneo makubwa ya mashamba yaliteketea na kuwekewa mabomu ya ardhini, na sehemu ya mashariki ya nchi ikawa chini ya uvamizi wa Urusi.

Hii ilisababisha kupotea kwa uwezo wa uzalishaji, kuvurugika kwa mifumo ya usafirishaji wa bidhaa, kupungua kwa uzalishaji, na kufanya iwe vigumu kusambaza bidhaa ambazo hapo awali zilikuwa sehemu ya mauzo ya nje ya Ukraine. Kwa sababu hiyo, muundo wa uhusiano wa kiuchumi na kibiashara wa Ukraine na Kenya na Malaysia ulibadilika.

Katika mwaka wa 2021, biashara ya bidhaa kati ya Ukraine na Kenya ilikuwa na thamani ya dola milioni 214.78, ambapo mauzo ya Ukraine kwenda Kenya yalifikia dola milioni 196.74 na uagizaji kutoka Kenya ulikuwa dola milioni 18.04. Kufikia mwaka wa 2024, thamani ya biashara kati ya nchi hizo mbili ilikuwa imeshuka hadi dola milioni 159.01. Mauzo ya Ukraine kwenda Kenya yalishuka hadi dola milioni 4.53, huku uagizaji kutoka Kenya ukiongezeka hadi dola milioni 154.48.

Biashara na Malaysia pia ilipata anguko kubwa baada ya kuanza kwa uvamizi kamili, ingawa baadaye ilianza kuimarika. Kufikia mwisho wa mwaka wa 2024, biashara kati ya Ukraine na Malaysia ilikuwa na jumla ya dola milioni 383.6, ikijumuisha mauzo ya Ukraine yenye thamani ya dola milioni 103.82 na uagizaji wenye thamani ya dola milioni 279.78

Nini kilitokea kwa biashara na kilimo cha Donbas baada ya uvamizi

Kiwanda cha Azovstal Iron and Steel Works mjini Mariupol, mkoa wa Donetsk, kilikuwa miongoni mwa wazalishaji wakubwa wa chuma ghafi barani Ulaya. Baada ya kuanza kwa uvamizi kamili, kiwanda hicho kikawa ngome muhimu katika ulinzi wa jiji. Wakati wa vita kali kati ya tarehe 18 Machi na 16 Mei 2022, kituo hicho kilikumbwa na mashambulizi makubwa ya anga, mizinga na makombora kutoka Urusi, yaliyoharibu karibu kila miundombinu yake ya uzalishaji na utawala.

Baada ya Mariupol kutekwa, mamlaka za Urusi hazikujenga upya kiwanda hicho kutokana na ukubwa wa uharibifu.

Kampuni nyingine kubwa ya viwanda nchini Ukraine ilikuwa Illich Iron and Steel Works ya Mariupol. Kabla ya uvamizi kamili, bidhaa zake zilisafirishwa katika zaidi ya nchi 50 duniani.

Katika mwaka wa 2022, wakati wa uvamizi wa Mariupol na majeshi ya Urusi, kiwanda hicho kiliharibiwa kwa kiasi kikubwa. Vikosi vya uvamizi vilisafirisha vifaa vilivyokuwa bado salama kwenda Urusi na kuuza miundo ya chuma na mashine zilizoharibiwa kama chuma chakavu . Licha ya hali hiyo, mamlaka za uwakilishi hutangaza mara kwa mara nia ya kuanzisha upya shughuli.

Kiwanda cha Alchevsk Iron and Steel Works kilikuwa miongoni mwa viwanda vikubwa vya metallojia ya metali za feri nchini Ukraine, kikibobea katika uzalishaji wa chuma ghafi na bidhaa za chuma zilizovingirishwa. Kinapatikana katika mji wa Alchevsk, mkoa wa Luhansk, ambao umekuwa chini ya uvamizi wa Urusi tangu mwaka wa 2014.

Baada ya mji huo kuvamiwa, Urusi “ilitaifisha” kiwanda hicho. Ingawa kituo hicho kinaendelea kufanya kazi, shughuli zake zinakabiliwa na changamoto kubwa za upatikanaji wa malighafi, usafirishaji na uuzaji wa bidhaa. Kwa sababu hiyo, uzalishaji wake bado uko chini sana ya viwango vya kabla ya uvamizi.

Hali ya sekta ya kilimo katika mikoa ya Luhansk na Donetsk — ambayo ilikuwa na mchango mkubwa katika jumla ya mauzo ya nje ya Ukraine kwenda nchi za Asia na Afrika kabla ya uvamizi wa kijeshi wa Urusi — bado ni mbaya sana. Kutokana na uvamizi wa Urusi, Ukraine ilipoteza fursa ya kufikia sehemu kubwa ya mashamba yake, jambo lililofanya kilimo, upandaji wa mazao na uvunaji kutowezekana.

Katika maeneo ya mkoa wa Donetsk ambayo bado yako chini ya udhibiti wa Ukraine, wakulima wanaendelea kulima mazao ya nafaka na mbegu za mimea ya mafuta. Hata hivyo, ukaribu na eneo la vita pamoja na mashambulizi ya mara kwa mara — ambayo husababisha mashamba kuwekewa mabomu ya ardhini na kuteketea — vinatatiza sana shughuli za kilimo na kupunguza mavuno.

Je, uhusiano wa kiuchumi kati ya nchi hizi unaendelea katika mwaka wa 2026?

Vita vimebadilisha kwa kiasi kikubwa uwezo wa Ukraine wa uzalishaji wa kilimo na viwandani, hasa katika mikoa ya Luhansk na Donetsk. Uharibifu wa viwanda vya chuma, uvamizi wa maeneo na kupotea kwa uwezo wa uzalishaji pamoja na mashamba kumeathiri muundo wa mauzo ya nje ya Ukraine, haswa kwenda Kenya na Malaysia.

Kabla ya uvamizi wa kijeshi wa Urusi, Donbas ilikuwa mchangiaji mkuu wa uzalishaji wa chuma na kilimo katika usafirishaji wa jumla wa bidhaa za nje za Ukraine. Leo, bidhaa zinazotumwa na Ukraine kwenda katika nchi hizi zinajumuisha zaidi bidhaa za kilimo na chakula zinazozalishwa katika maeneo mengine ya Ukraine.

Licha ya vita na athari zake, Ukraine inaendelea kudumisha ushirikiano wa kibiashara na kiuchumi na Kenya na Malaysia.

Katika mwaka wa 2026, kupitia mpango wa kibinadamu wa Rais wa Ukraine wa ‘Food from Ukraine’, Ukraine ilisafirisha shehena ya chakula yenye tani 2,618.15 kwenda Kenya. Jumla ya kiasi cha shehena ya misaada ya kibinadamu kilizidi tani 3,600. Zaidi ya hayo, Ukraine iliwasilisha nafaka kwa Kenya kupitia mpango wa kibinadamu wa ‘Grain from Ukraine’.